Friday, March 27, 2009

MALECELA AANZA KUNYONGA DEMOKRASIA TANZANIA

KWA NINI WANANCHI WENGINE WASIWE NA MAWAZO YA KUTAKA KUGOMBEA NAFASI YA URAIS WAKATI KATIBA INARUHUSU WAZI KABISAAAAA???!!!!??


http://www.ippmedia.com/ipp/images/2009/03/26/134062.jpg

CCM Central and National Executive Committee member John Malecela gestures at a press conference held at his residence in Dar yesterday, where he condemned the exchange of words between some party members, parliamentarians and the media.

2009-03-26 12:38:03
Na Joseph Mwendapole

Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, John Malecela, amesema kuwa mwanachama yeyote wa CCM atakayejitokeza kuchukua fomu kupambana na Rais Jakaya Kikwete katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, atakuwa anapoteza muda wake.

Yeye binafsi ameweka msimamo wake wazi kuwa hatajitokeza kuchukua fomu kugombea kiti cha urais mwakani tofauti na alivyofanya mwaka 1995 na mwaka 2005 na jina lake kuondolewa na vikao vya Kamati Kuu (CC) ya chama hicho.

Alisema mwanachama wa CCM mwenye fikra hizo ni vyema akazifuta mapema na atumie fedha ambazo angetumia kwenye kampeni za urais kuendeleza familia yake.

Aliyasema hayo jana nyumbani kwake Sea View, jijini Dar es Salaam, wakati akizungumza na waandishi wa habari kutoka vyombo vya habari vya IPP.

Alitoa jibu hilo baada ya kuulizwa iwapo atawania urais mwaka 2010 baada ya jina lake kuchujwa katika kinyang`anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005.

``Rais Kikwete ameifikisha nchi sehemu nzuri sana, hakuna wa kumpiku, ametuendesha vizuri tangu tumpe usukani mwaka 2005 na lazima wananchi na wanachana wa CCM wajue kuwa mwaka 2010 ni kituo tu Kikwete hajafika mwisho....mwisho wake wa urais ni 2015,``alisema na kuongeza kuwa yeye hatagombea urais badala yake ataendelea kuwania ubunge katika jimbo lake la Mtera, mkoani Dodoma.

Alipoulizwa kuhusu dhamira yake kutokana na kuondolewa na Kamati Kuu (CC) ya chama hicho katika kinyang`anyiro cha urais mwaka 2005 na kuamua kukata rufaa Halmashauri Kuu (NEC), alisema hadi sasa hana kinyongo.

Alikemea malumbano yaliyotokea hivi karibuni baina ya Mbunge wa Igunga (CCM), Rostam Aziz, na Mbunge wa Kyela (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe, kuhusu mjadala wa ununuzi wa mitambo ya Dowans.

Alisema wakati huu wa hali mbaya ya kiuchumi, viongozi wanapaswa kuweka mikakati ya kumsaidia Rais Kikwete ambaye amekuwa akiizunguka dunia kutafuta misaada ya Tanzania, badala ya kuendekeza malumbano.

Alisema badala ya kulumbana hadharani, wanapaswa kupeleka masuala hayo katika Bunge, Serikali au katika chama.

``Kwa kweli tumechoshwa na malumbano haya, hakuna sababu ya kuendeleza malumbano kwani kama suala linahusu serikali kwanini lisipelekwe huko likajadiliwa?

Kama ni la Bunge, kwanini lisipelekwe bungeni? na kama ni la chama kwanini lisipelekwe kwenye chama mpaka watu wanasutana katika magazeti,`` alihoji Malecela ambaye pia aliwahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais kuanzia mwaka 1990 hadi 1995.

Alisema lipo kundi la watu wanaojidanyanga kuwa ipo siku CCM itameguka endapo watajitoa katika chama na aliwataka kufanya hivyo haraka iwezekanavyo.

Alisema hata wakiondoka chama kitabaki imara na hakitatetereka.

``Baba wa Taifa aliwahi kusema kuwa bila CCM imara nchi itayumba, lakini hakumaanisha kuwa chama hiki kitameguka, sasa hao ambao wamekuwa wakitoa vitisho kila kukicha kitameguka ni heri waondoke tumechoka na vitisho vyao,`` alisema.

Alisema CCM haitakubali watu wachache waruhusiwe kuiyumbisha nchi kwa sababu wanazojua wao.

Vile vile, Malecela alisema kamwe CCM haitaruhusu matajiri kuongoza chama hicho na kwamba wanaojaribu kufanya hivyo wanajidanganya.

Alisema chama hicho kitaendelea kuwa chama cha wanyonge na wafanyakazi.

Kuhusu mjadala wa Dowans, Malecela alisema ni sawa na kuchapa bakora mzoga kwani suala hilo lilishajadiliwa na kumalizwa na Bunge.

Alisema anayeona mjadala huo unamaana tena anaweza kuwasilisha hoja yake bungeni.

Kuhusu madai ya wizi wa fedha za umma zinazomwandama Mbunge wa Bariadi (CCM), Andrew Chenge, Malecela alisema hizo ni tuhuma tu na kwamba Mahakama pekee ndiyo yenye uwezo wa kumtia hatiani.

Alisema mtu yeyote anaweza kutuhumiwa hivyo haoni ajabu kwa yanayosemwa kuhusu mwanachama huyo wa CCM.

``Watuhumiwa wako wengi hapa nchini na hata wewe unaweza kuwa mtuhumiwa wakati wowote tu na kisheria mtuhumiwa hana hatia mpaka Mahakama itakapomwona na hatia,`` alisema.

Wakati huo huo, Malecela, ameishauri serikali iyafunge magazeti ambayo yamekuwa yakiandika uongo na mambo binafsi dhidi ya watu mbalimbali.

Alisema magazeti hayo yanakosa habari na badala yake yanaandika uongo na uzushi.

``Imefika wakati sasa serikali ifanye kazi yake...magazeti haya sasa yamekuwa mengi mno na yamefikia hatua mbaya ya kuandika mambo ya uongo,`` alisema Malecela.

Aliongeza kuwa serikali isiendelee kuyafumbia macho na kwamba lazima ionyeshe kuwa haikubaliani nayo kwa kuchukua hatua madhubuti ikiwa ni pamoja na kuyachuja.

Alisema mpaka sasa ripoti zinaonyesha kuwa Tanzania ina magazeti mengi kuliko nchi yoyote barani Afrika.

``Imefikia wakati yanaingilia mambo ya watu binafsi ya ndani kabisa na kuyachapisha..lazima tujiulize haya yanafanyika kwa faida ya nani?`` alihoji.

Aidha, alisema kuwa anaamini vyombo vya habari vimeanzishwa kwa ajili ya kuelimisha umma na si kuandika uongo na kuendeleza malumbano.

Alitahadharisha kuwa hali hiyo ikiendelea, wananchi wanaweza kudhani kuwa uhuru wa vyombo vya habari ni watu kutukanana na kukashifiana.

Hivi karibuni, kumeibuka kundi la magazeti ambayo yamekuwa yakishambulia watu wanaopambana na ufisadi.

Magazeti hayo yamekuwa yakiandika habari za uongo na za kutunga dhidi ya watu wanaomuunga mkono Rais Kikwete katika kupambana na vitendo vya ufisadi.

· SOURCE: Nipashe


No comments:

Post a Comment