Sunday, March 1, 2009

MICHANGO YA KUCHARAZWA BAKORA WALIMU

2009-02-17 13:12:53
Na Hamisi Kibari
Niliposikia kwa mara ya kwanza kwamba Mkuu wa Wilaya ya Bukoba mkoani Kagera ameamrisha askari kuwacharaza bakora waalimu, swali nililiomuuliza mtu aliyenipa habari hiyo kwa mara ya kwanza lilikuwa hili: ``Huyo mkuu wa wilaya ni mzima kweli kiakili?``
Niliuliza swali hilo kabla hata sijataka kujua sababu za uamuzi huo.

Yule mtoa habari wangu alijibu: \"Pengine ni mzima tu isipokuwa amelewa madaraka... Unajua madaraka na fedha wakati mwingine huwafanya watu wafanye mambo ya ajabu.``

Kwangu mimi, mwalimu kuamriwa achapwe viboko huku wanafunzi wake wakiona au kusikia kwa mbali, hata ungesema amefanya kosa gani ambalo si la kuua mtu, siwezi kukuelewa.

Binafsi nilifarijika kwa hatua alizochukua Rais Jakaya Kikwete, kumtimua kazi mkuu huyo wa wilaya, Albert Mnali.

Nimesikia pia kwamba hatua hiyo ya Kikwete imewagawa wananchi mkoani Kagera. Nimesikia wapo hata wale ambao wanataka kuandamana kupinga kufukuzwa kazi kwa mkuu huyo wa wilaya.

Mimi kama mzazi, ninajua inavyouma kwa mtoto wako kutofaulu mitihani wa kuvuka ngazi moja kwenda nyingine, huku sababu kubwa ikiwa ni uzembe wa walimu.

Lakini pamoja na hayo, DC kuamrisha adhabu ya walimu kuchapwa viboko, inashangaza sana. Inafuta mazuri yake yote, kama yapo, aliyofanya na hivyo adhabu ya kutimliwa kazi ni mwafaka.

Kwa adhabu hiyo, waalimu waliowatendewa `unyama` wanapata faraja angalau kidogo na inawafanya wengine wenye tabia inayoweza kuvuka mipaka yao ya kazi kuwa makini zaidi.

Hakuna ubishi kwamba bwana huyu alilewa madaraka kama alivyonijibu yule mtoa habari wangu kwa sababu, licha ya kukiuka katiba, alikiuka hata kanuni za utumishi wa umma.

Kuhusu Katiba, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ikimlalamikia DC huyo ilisema kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977 na mikataba ya kimataifa inayolinda haki za binadamu na misingi ya utawala bora ambayo Tanzania imeridhia inakataa kabisa alichokifanya Mnali.

Ikikariri Ibara ya 13 (6) (e) Tume ilisema ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama ama kupewa adhabu zinazomtweza na kumdhalilisha. Tume iliendelea kusema kwamba adhabu ya viboko hutolewa na mahakama peke yake, tena kwa kosa la jinai linaloainishwa kisheria.

Na kama alivyosema Rais katika hatua ya kumfukuza kazi Mnali, kanuni za utumishi wa umma zinasema kwamba kamati za nidhamu za wilaya na mikoa ndizo zenye jukumu la kumuadhibu mtumishi.

Mbali na madai ya kuchelewa kazini, inaelezwa kwamba Mnali alichukua hatua hiyo kwa kukerwa na wilaya yake kuwa nyuma kutokana na shule nyingi kutofanya vizuri katika kushindisha watoto kwenda sekondari.

Kimsingi, hatua ya watoto kufeli inakera, si tu kwa wazazi bali hata kwa viongozi kama Mnali na inahitaji kuchukuliwa hatua. Lakini hebu tujiulize; kweli kuwachapa walimu bakora ni njia sahihi ya kumaliza tatizo la wanafunzi kufeli darasani? Jibu bila shaka ni hapana.

Mnali alitakiwa kuchunguza chanzo cha wanafunzi kufeli, ambacho hakiwezi kuwa uchelewaji wa waalimu peke yake, kisha akatafuta njia za kumaliza tatizo hilo. Hili si jambo la kukurupuka wala kulimaliza kwa kutumia msuli, kufumba na kufumbua, bali ni kukaa chini na kushirikiana na watalaamu mbalimbali wilayani, hususan maofisa elimu, katika kusaka ufumbuzi.

Je, nini tumejifunza katika sakata hili? Bila shaka yako mengi, lakini mimi nimegundua mawili ambayo ningependa kuyatolea angalizo.

La kwanza ni umuhimu wa kuchukua hatua haraka pale kiongozi wa umma anapolewa madaraka na \'kunajisi\' ofisi, kama alivyofanya Rais Jakaya Kikwete katika kumfukuza kazi Mnali.

Pamoja na kwamba mambo mengine yanahitaji uchunguzi kabla ya hatua kuchukuliwa, lakini siku zote yapo ambayo hayahitaji kusubiri kama hili la Mnali, hasa ikizingatiwa kwamba wapo Watanzania lukuki wanaoweza kuongoza wilaya.

Viongozi wetu wanatakiwa wakati mwingine kuchukua maamuzi magumu na ya haraka kunapokuwa na jambo linalolalamikiwa na wananchi badala ya kulindana ama kusuasua.

La pili ambalo mimi nimejifunza ni kuungana na wale ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakishauri nyadhifa hizi za ukuu wa wilaya na mkoa, zisitolewe kisiasa hata kama viongozi hawa wanaitwa wawakilishi wa Rais.

Rais kwa kushirikiana na wasaidizi wake, hususan Waziri Mkuu hawezi kuwajua Watanzania wazuri waliotapakaa nchi nzima wenye sifa za kushika nyadhifa hizi na wakasaidia kusukuma maendeleo ya nchi mbele.

Mimi siungani sana na wale ambao wangependa nafasi za ukuu wa wilaya ama mkoa ziwe za kugombea kama ubunge, bali mimi ninaungana na wale wanaopendekeza zitangazwe, na wenye sifa waombe.

Huko nyuma, kwa mfano, chama cha mpira wa miguu nchini kiliendeshwa na katibu mkuu wa kuchaguliwa. Sasa hivi kinaendeshwa na mwajiriwa, aliyeomba na kuchaguliwa kutokana na sifa na uwezo wake ambapo akikiuka yale anayotakiwa kufanya anafukuzwa kazi.

Mimi ninaona kana kwamba mambo yanakwenda vizuri zaidi TFF kuliko zamani. Vivo hivyo, ingekuwa kwa wakuu wa wilaya na mikoa.

Nafasi ya mkuu wa wilaya ama mkoa ni nyeti. Zinataka watu wenye sifa ambao hawawezi kufanya mambo ya ajabu kama aliyofanya Mnali.

No comments:

Post a Comment