Tuesday, August 21, 2012

CCM IMEINGIZA NCHINI TANZANIA SILAHA BILA VIBALI?

Dk. Slaa ‘anasa’ silaha za CCM -  Posted here on 22/8/2012

na Abdallah Khamis, Morogoro
KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, ameibua tuhuma nzito dhidi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), akidai kimeingiza silaha nchini bila ya vibali ili zitumiwe na vijana wao kukabiliana na wapinzani.
Dk. Slaa alisema kuwa wanazo nyaraka zinazoonesha namna CCM walivyoingiza silaha hizo nchini kwa ajili ya kuwapatia vijana wao waliowekwa kwenye makambi maalumu wakipatiwa mafunzo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Morogoro, kuelezea tathmini ya Operesheni Sangara, maarufu kama Vuguvugu la Mabadiliko (M4C) inayoendelea mkoani humo, Dk. Slaa alisema mbinu hizo zimekuwa zikitumiwa muda mrefu na viongozi wa CCM.
Alitolea mfano kauli ya Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama, aliyoitoa wakati wa uchaguzi mdogo jimboni Igunga akidai kuwa CHADEMA imeingiza askari wenye mafunzo maalumu nchini.
“Nilikuwa ninajiuliza hawa CCM wana ujasiri gani wa kusema uongo kwa vyama vingine juu ya kuingiza silaha, sasa nimejua dhamira yao baada ya kupata nyaraka zinazoonesha mpango mkakati wao wenye lengo la kuwatumia vijana walio katika makambi yao kwa ajili ya kufanya vurugu kwa kutumia silaha wanazowapatia,” alisema.
Aliongeza kuwa kudhihirisha CCM hawatanii katika kutaka kufanya vurugu, msafara wa CHADEMA mkoani humo umekuwa ukiandamwa na watu tofauti kwa kutumia magari tofauti.
Dk. Slaa alibainisha kuwa juzi wakiwa wanatoka katika Jimbo la Gairo, gari lenye namba za usajili T 886 AVS aina ya Prado lilikuwa likiwafuatilia hadi wilayani Mvomero na taarifa hizo walizitoa kwa askari waliokuwa wakilinda mikutano yao katika Wilaya ya Mvomero.
“Juzi walifanya hivyo tukiwa Mvomero, tukatoa tarifa polisi na leo asubuhi tumepata taarifa ambazo hatuwezi kuzipuuza kuwa kuna vijana kati ya 10-20 wakiwa na sumu, sindano na visu wanawawinda watu walio katika operesheni kwa ajili ya kuwadhuru na nimewaagiza vijana wangu wa idara ya usalama wakatoe taarifa polisi,” alisema Dk. Slaa.
Hata hivyo, wakati Dk. Slaa akisema taarifa za msafara wao kufuatiliwa wakiwa wanatoka Gairo kuelekea Mvomero, waliziwasilisha polisi ili zifanyiwe kazi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, alisema hana taarifa hizo.
Nape akanusha
Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC) Taifa wa CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alikanusha tuhuma za Dk. Slaa, akidai kuwa mwanasiasa huyo anazeeka vibaya na kwamba ni bora akawaachia vijana siasa.
“Maneno haya hayapaswi kusemwa na mtu kama Dk. Slaa lakini nikwambie kuwa CCM haina makambi hayo anayoyasema, naomba Watanzania wampuuze,” alisema.
Nape aliongeza kuwa CCM haijawahi kuwaza kuwa na mawazo ya kutumia silaha na haitakuwa nayo kama alivyodai Dk. Slaa, akibainisha kuwa hata wakati wa kudai uhuru silaha hizo hazikutumika.
Alisema kuwa anachokiona ni kwamba CHADEMA inasambaratika na hivyo inaanza kutafuta sababu za uongo, huku akikumbushia madai aliyoyatoa Dk. Slaa mwaka juzi wakati wa Uchaguzi Mkuu kuhusu wizi wa kura.
“Utakumbuka mwaka 2010 wakati wa Uchaguzi Mkuu, Dk. Slaa alisema kuna kontena lina kura mkoani Mbeya, lakini hadi leo hajawahi kuthibitisha uongo wake,” alisema Nape.
Pinda abanwa
Katika hatua nyingine, Dk. Slaa amemtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuweka hadharani michango iliyokusanywa kwa ajili ya waathirika wa matukio ya mabomu ya Gongo la Mboto na Mbagala; na mafuriko ya Kilosa na Dar es Salaam.
Dk. Slaa alisema waziri mkuu anapaswa kutoa maelezo ya kina ndani ya siku 30 ili Watanzania wajue michango waliyochanga kwa ajili ya kuwasaidia ndugu zao ni kiasi gani na imetumikaje.
Alisema baada ya waziri mkuu kutoa hesabu ya vitu vilivyokusanywa pia anapaswa kumuagiza Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuvifanyia ukaguzi ili kujua namna vilivyotumika na kwamba kama hilo litashindikana, wabunge wa CHADEMA watakuwa na wajibu wa kuandaa hoja binafsi na kuiwasilisha bungeni.
“Tumeshuhudia namna waathirika wa mafuriko ya Kilosa walivyochangiwa na Watanzania kutoka sehemu tofauti ya nchi, sasa leo wamefikia kulazwa chini chumba kimoja kwa familia nzima pasipo kujali umri wala jinsia na mbaya zaidi, vyoo wanavyotumia havina milango, huku ni kufedhehesha utu wa Mtanzania,” alisema.
Wavuna wanachama 31,337
Wakati huo huo, Mkuu wa Operesheni Sangara wa CHADEMA katika mikoa mitano ya Morogoro, Singida, Manyara, Dodoma na Iringa,  Benson Kigaila, alisema baada ya kupita katika majimbo sita ya mkoani Morogoro wamefanikiwa kuvuna wanachama 31,337.
Kigaila alisema wanachama hao ni baada ya CHADEMA kufika katika kata 137 na vijijji 471 kwenye majimbo sita ya mkoa huo. Kwamba alipokea kadi 7,603 kutoka katika vyama vingine.
Alisema katika operesheni hiyo, wananchi walichangia kiasi cha sh 17,895,650, ndizi mikungu 831, magimbi 73, mayai trei 17 na mchele kilo 148.
Kigaila alifafanua kuwa kadi zilizouzwa ziliingiza kiasi cha sh 15,768,500.


--

No comments:

Post a Comment