Thursday, September 6, 2012

NAMNA YA MUUNGANO UTAKIWAO TANZANIA NA ZANZIBAR


Toleo la 257
5 Sep 2012
MOJA ya mambo yenye kushangaza katika mjadala unaoendelea Zanzibar kuhusu Muungano wa Tanzania ni ile dhana ya kwamba upinzani dhidi ya muundo wa sasa wa Muungano ulianza jana au kwamba umekuwa ukichochewa na mtu fulani au kikundi fulani chenye ‘ajenda ya siri.’
Ukweli wa mambo ni kwamba Muungano uliasisiwa katika mazingira ya kutatanisha na hivyo tangu siku ya mwanzo ya kuzaliwa kwake ni wachache Zanzibar waliousherehekea kwa moyo mkunjufu.
Wengi walikuwa na dukuduku na waliingiwa na wahasha lakini hawakuwa na la kufanya.  Wajumbe kadhaa wa Baraza la Mapinduzi la awali wameniambia kwamba lau suala hilo lingejadiliwa kwa uwazi katika Baraza hilo na lau wajumbe wa Baraza wangepewa fursa ya kuamua basi wangeliupinga muundo huo wa Muungano.
Hawasemi kwamba wangelipinga kuwapo kwa aina ya umoja au shirikisho baina ya Tanganyika na Zanzibar, lakini wangepinga muundo ulioibuka wa Muungano wa nchi hizo mbili. Tukumbuke kwamba wakati huo Baraza la Mapinduzi ndilo lililokuwa na majukumu ya utungaji wa sheria za Jamhuri ya Watu wa Zanzibar.
Wenye kuhoji (bila ya kutoa hoja madhubuti) kwamba wenye kuupinga muundo wa Muungano wana ajenda ya siri ya kurejesha usultani wanajikanganya na kujisuta wenyewe.
Sijui Sheikh Abeid Karume, mmoja wa waasisi wa Muungano huu, alikuwa na ajenda gani ya siri alipokuwa akiupiga vijembe Muungano katika siku za mwisho za uhai wake. Wakati huo alikuwa amekwishatanabahi kwamba muundo wa Muungano kama ulivyo haukuwa na manufaa kwa nchi yake. Ndiyo maana akatamka kwamba ‘Muungano ni kama koti likikubana unalivua’.
Wakati mwingine siku moja tu kabla hajaiaga dunia alimwambia Bwana Salim Rashid, katibu mkuu wa kwanza wa Baraza la Mapinduzi, kwamba Muungano ni kama matoto ya treni na Zanzibar inashikilia shoka ambalo karibu italitumia kuukata mnyororo unaoyaunganisha hayo matoto na ukikatika kila toto litakwenda upande wake. Kwa hayo alikuwa na maana kwamba Tanganyika ingekwenda upande wake na Zanzibar ingekwenda upande wake.
Wala sijui kina Kanali Seif Bakari na wenzake na tepu zao za ‘Kiroboto’ zilizokuwa zikitangazwa Redio Zanzibar walikuwa na ajenda gani na ya kumrejesha sultani gani Zanzibar.
Ninachojaribu kukumbusha ni kwamba upinzani dhidi ya muundo wa Muungano haukuanza jana wala leo. Lililo muhimu zaidi ni kutambua kwa kujikumbusha kwamba upinzani huo ulijikita pia ndani ya duru za waliokuwa wakihodhi madaraka Visiwani Zanzibar baada ya Mapinduzi ya mwaka 1964.
Viongozi hao wa Mapinduzi walikuwa na imani thabiti na ile sera ya kutaka kuleta umoja barani Afrika lakini kwa namna mambo yalivyokuwa yakienda baada ya kuundwa Muungano walianza kuukosoa muundo wa Muungano huo.
Mara kadha wa kadha katika uhai wake wa miaka 48 Muungano wetu umekuwa ukikabiliwa na mikwaruzano ya aina kwa aina.
Kwa mfano, kuna kile kisa kilichosababisha Sheikh Aboud Jumbe kupokonywa wadhifa wake wa kuwa Rais wa Zanzibar mnamo mwaka 1984 alipojaribu kuirejeshea Zanzibar mamlaka yake kamili ya utawala. Aling’olewa madarakani kwa nazaa na Chama cha Mapinduzi (CCM) na wala si na Baraza la Mapinduzi kama ilivyotakiwa na Katiba ya Zanzibar.
Ni muhimu tuwe tunakumbuka kuwa Wazanzibari hawakuanza kudai mabadiliko ya muundo wa Muungano baada ya kuanza mchakato wa sasa wa kulitafutia taifa Katiba mpya lakini walianza kunung’unika tangu miaka ya 1960 walipogutuka na kuona kwamba muundo wa Muungano hauwapi fursa waitakayo ya kujiamulia mambo yao na kuyatetea maslahi yao.
Ndiyo maana kila walipopata fursa ya kutoa maoni yao juu ya Muungano, kama kwa mfano, wakati wa Tume za Nyalali na Kisanga Wazanzibari wengi walipendelea pawepo na mfumo wa serikali tatu katika Muungano.Waliamini kwamba mfumo huo ungeirejeshea Zanzibar mamlaka yake yaliohamishiwa Bara.
Tusisahau pia kwamba si zamani sana ilikuwa ni kosa, tena la uhaini, kwa Mtanzania ‘kuujadili’ Muungano kadamnasi, seuze kupendekeza mageuzi katika muundo wake au kupendekeza kwamba uvunjwe kabisa.
Juu ya kuwako vipingamizi hivyo Wazanzibari wameendelea kuwa wavumilivu lakini hawakusita kuyakosoa yale mambo yenye kuyadhuru maslahi yao ya kitaifa.
Wale wenye kufikiri kwamba msimamo wa Wazanzibari juu ya Muungano ni wa karibuni pamoja na kampeni inayopigwa Visiwani ya kutaka mageuzi ya kimsingi kuhusu Muungano hawaiangalii historia ipasavyo.
Wangeitalii historia ipasavyo wangeona kwamba hata katika vikao mbalimbali vya Baraza la Wawakilishi tokea miaka ya 1980 suala la Muungano lilikuwa likiibuka mara kwa mara na kwamba Baraza hilo kila lilipopata fursa lilikata maamuzi yenye kutetea maslahi ya Zanzibar. Mifano ya hivi karibuni ni pamoja na yale maamuzi yanayohusika na masuala ya mafuta na gesi asilia.
Tumeshuhudia pia kwamba kila siku zikisonga mbele Baraza la Wawakilishi limekuwa likizidi kupaza sauti yake kuhusu msimamo wake juu ya Muungano. Limekuwa likifanya hivyo hata kabla ya mchakato wa sasa wa Katiba kuanza.
Hivyo ni kosa na upotoshaji wa hali ilivyo kudai kwamba ni jumuiya, chama au mtu fulani mwenye kuwachochea au kuwahamasisha Wazanzibari wawe na msimamo fulani juu ya Muungano.
Tuseme tu kuwa mazingira ya sasa yanawawezesha Wazanzibari kutoa maoni yao kwa uwazi zaidi bila ya kuingiwa na hofu. Hii leo sheria haitomtia nguvuni mtu anayetoa maoni ya kutaka muundo wa Muungano ubadilishwe au hata anayetaka Muungano wenyewe uvunjwe.
Hofu hiyo ilikuwapo zamani hata pale uliporejeshwa tena mfumo wa vyama vingi vya kisiasa kwani Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema kwamba vyama vipya vya kisiasa vinaweza kujadili masuala yote lakini visiuguse Muungano.
Hivyo, wengi walitishika kuukosoa Muungano wakiamini kwamba ilikuwa ni uhaini kufanya hivyo kutokana na maneno ya Mwalimu.
Si ajabu kuwaona Wazanzibari wakiwa na hofu hiyo kwani kwa jumla Watanzania wote waliteseka chini ya mfumo wa chama kimoja cha kisiasa kuanzia mwaka 1964 hadi 1992.
Kadhalika, kwa muda wa miaka 28 kati ya 48 ya Muungano, CCM ikiwa na makao yake makuu mjini Dodoma, ndiyo iliyokuwa ikishika mpini kuhusu masuala ya Muungano kama vile kwa mfano wakati wa kutungwa Katiba ya Muungano mwaka 1977.
Sasa hali ya mambo imebadilika na ndiyo maana wakati wa kutoa maoni yao mbele ya Tume ya Warioba kuna Wazanzibari wanaosema kuwa wanataka pawepo Muungano wa Tanganyika na Zanzibar utaojengeka juu ya msingi wa Mkataba na si Katiba.
Katika Muungano wa aina hiyo kila nchi itakuwa na mamlaka kamili ya utawala wa mambo ya ndani ya nchi yake pamoja na shughuli za kigeni au za kimataifa. Mfumo huo ni bora zaidi kushinda ule wa serikali tatu ambao wengi wanauona kuwa umepitwa na wakati na uliokwishakataliwa na Serikali za Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Kadhalika, kuna uwezekano mkubwa kwamba muundo wa aina hiyo utaweza kuzivutia nchi nyingine katika kanda ya Afrika ya Mashariki na ya Kati kujiunga na Muungano wetu na hivyo kuimarisha kidhati Umoja wa Kiafrika.
Hapana shaka yoyote kwamba Muungano wa aina hiyo utakuwa imara na wa maana zaidi kinyume na huu wa sasa ulioselelea kuwa wa nchi mbili tu takriban nusu karne baada ya kuasisiwa na usiokwisha kukumbwa na mikwaruzano na kero za kila aina.
Kwa hakika historia ya Muungano itapoandikwa kwa dhati na bila ya upendeleo itaonyesha kwamba Zanzibar daima imekuwa na dukukudu kuhusu nafasi yake ndani ya huu Muungano baina yake na Tanganyika. Historia hiyo itaonyesha pia kwamba kuna Wazanzibari wenye kuamini kwamba wameonewa katika mahusiano kati ya nchi yao na Tanganyika.
Ili kuondosha chokochoko zilizopo na kuondosha ukinzani uliopo kati ya pande mbili za Muungano kuna haja ya kuwa na muundo wa Muungano utaoziridhisha pande zote mbili na utaoweza kuzifuta kabisa na kwa njia za amani na udugu tofauti zilizopo kati yao kwa manufaa ya Watanganyika na ya Wazanzibari.
Kama kweli tunataka bara la Afrika liungane kiuchumi, kisiasa na kijamii basi kuna ulazima kwamba misingi ya umoja huo iwe madhubuti na iziwezeshe nchi zinazoungana ziungane kila moja ikiwa na mamlaka kamili ya kujiamulia mambo yenye kuhusika na maslahi yake.
Muungano aina hiyo utafana endapo tu utakuwa ni wa hiyari na si wa kulazimishwa na ikiwa utaipa kila nchi iliyomo ndani yake haki ya kuwa na kauli sawa na uhuru wa kujiamulia yaliyo yake bila ya kuyadhuru maslahi ya nchi nyingine zilizo ndani ya Muungano huo.

No comments:

Post a Comment