Saturday, September 22, 2012

LINDI YAWEZA KUWA SRI LANKA [CEILON] YA TANZANIA

Imeingizwa humu tarehe 23/9/2012.
 
Lindi yaweza kuwa Sri Lanka ya Tanzania


 


 
 
 


 


Toleo la 259
19 Sep 2012

WATANZANIA wengi tukisikia jina Sri Lanka jambo kubwa linalotujia kwa haraka ni ama chai au Vita ya Tamil Tigers. Nakumbuka tulipokuwa darasa la sita Shule ya Msingi tulisoma ‘Chai Sri Lanka’ na kusoma miji kama Kolombo, Batikaloa na Trinkomalee (Colombo, Batticaloa, Trincomalee). Lakini tulipashwa sana habari kuhusu vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka takribani 30. Juzi nilikuwa Sri Lanka. Vita imekwisha mwaka 2009. Chai ipo nyingi sana. Mwaka 2010, Sri Lanka iliuza nje jumla ya tani 314,000 za chai yenye thamani ya dola za Marekani bilioni 1.37 na hivyo kuongoza duniani kimapato ingawa Kenya ilisafirisha chai nyingi zaidi, tani 441,000.
Hata hivyo, kutokana na ubora wa zao hilo kuwa chini kidogo Kenya ilipata dola za Marekani milioni 800 tu. Mwaka huo Tanzania, yenye eneo kubwa zaidi la kulima kuliko nchi zote hizo, iliuza nje tani 34,000 tu na kupata dola za Marekani milioni 61 hivi. Licha ya kwamba Tanzania ni nchi ya nne kwa kuzalisha chai Afrika baada ya Malawi, Uganda na Kenya, bado inaweza kuwa katika nafasi ya juu duniani iwapo tukiamua kuwa makini katika mambo tunayofanya na kupenda kufanya mambo makubwa.
Siku hizi napenda kujua historia za nchi katika kupambana na umasikini wa watu wao. Lengo ni kuelewa juhudi za nchi mbalimbali katika kuleta maendeleo ya watu na kujifunza pale ambapo nchi zimefanikiwa. Ukitembea mitaa ya Jiji la Colombo unaona mji mzuri msafi uliopangwa vema na kila mtu anaonekana kushughulika. Njia nzuri ya kujua ukweli wa maisha ya watu ni kuzungumza nao.
Mara nyingi hutumia madereva wa teksi au bajaji kwa jiji kama la Colombo. Katika mazungumzo na baadhi ya madereva wa bajaji nilizokuwa natumia pale Colombo niliona mwelekeo mmoja, kwamba katika kipindi cha miaka 10 iliyopita maisha yao yamebadilika sana. Wakisifia kuisha kwa vita dhidi ya Tamil Tigers na kuongezeka kwa mapato yao kwa watu kutumia zaidi usafiri. Dereva wa bajaji wa Jiji la Colombo anaingiza wastani wa rupia 4000 (shilingi 45,000) kwa siku. Nilitaka kujua nini chanzo cha mabadiliko haya ya kipato ambacho hadi wenye bajaji wanafaidika nayo. Takwimu zao zinaeleza mengi sana. Serikali iliamua kupambana na umasikini na hasa umasikini wa vijijini.
Mwaka 2002 asilimia 22.7 ya wananchi wote wa Sri Lanka walikuwa wanaishi chini ya mstari wa umasikini. Ilipofika mwaka 2011, kiwango cha umasikini kilikuwa asilimia sita tu. Umasikini ulishuka kwa kiwango kikubwa katika maeneo ya vijijini. Katika kipindi cha miaka mitatu kati ya mwaka 2007 mpaka 2010 umasikini wa wananchi wa Sri Lanka walio kwenye sekta ya chai (estate sector) ulishuka kutoka asilimia 32 ya waliokuwa wanaishi chini ya mstari wa umasikini mpaka asilimia 11.4 na wale wa vijijini nje ya sekta ya chai umasikini ulishuka kutoka asilimia 24.7 mpaka asilimia 9.4 katika kipindi hicho. Nilipouliza zaidi kwa wanasiasa na viongozi wa serikali nikaambiwa kuwa mabadiliko makubwa yaliyotokea miaka ya karibuni yalitokana na serikali kufanya uamuzi mahususi wa kuelekeza fedha nyingi zilizokuwa zinakwenda vitani kwenye uwekezaji vijijini. Wanasema walitumia fedha nyingi kwenye ruzuku ya mbolea kwa wakulima, kusambaza umeme vijijini na kujenga barabara za vijijini. Siku niliyofika niliona kwenye moja ya magazeti yao ya kila siku, rais wao akizindua mtambo wa kuzalisha umeme katika Mji wa Trincomalee uliopo mashariki mwa nchi hiyo.
Nikajiuliza mbona na sisi tunatekeleza MKUKUTA na tunasema kwamba tunawekeza fedha nyingi sana vijijini? Mbona na sisi tunatoa ruzuku ya mbolea yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 60 kwa mwaka? Inakuwaje wenzetu wafanikiwe sisi tusifanikiwe? Tanzania imeanza kutoa mbolea ya ruzuku katika msimu wa mwaka 2006/2007 kama ilivyo kwa Sri Lanka. Wenzetu katika miaka mitatu, kiwango cha umasikini kimepungua kwa asilimia 15 kwa wananchi walio katika sekta hiyo ya kilimo na wanaoishi vijijini. Sisi katika kipindi cha muongo mmoja, 2001 mpaka 2011, umasikini umepungua kwa asilimia mbili tu. Moja ya sababu ya sisi kushindwa ni kwamba mfumo wa mbolea ya ruzuku umegubikwa na ufisadi wa hali ya juu sana. Mfumo huu umedhihirisha namna ambavyo kazi ya kupambana na ufisadi ni ya kimfumo zaidi maana kwa namna viongozi wa vijiji wanavyoiba mbolea ya ruzuku, unaweza kiurahisi kabisa kusema rushwa ni sehemu ya utamaduni wa Mtanzania. Siamini hivyo. Ninaamini kwamba mfumo wetu unazalisha wala rushwa, walafi na watawala wenye tamaa na wasiotosheka kama nilivyoeleza katika makala zangu zilizotangulia. Je, tukiondoa ufisadi wa mbolea ya ruzuku tunaweza kupata mafanikio ambayo wenzetu wameyapata? Sina jibu wala jawabu la swali hili. Hata hivyo, ninaamini kwamba kutofanikiwa kwetu ni zaidi ya ufisadi. Ni kutofanya kazi kwa bidii? Ni kukosa umakini? Ni kutofurahia mafanikio? Ni kukosa uongozi thabiti unaoweza kusimamia mchakato wa maendeleo kuanzia ngazi ya kijiji mpaka Taifa?
Hebu tutazame pamoja takwimu hizi. Sri Lanka ina ukubwa wa kilometa za mraba 65,000. Mkoa wa Lindi una ukubwa wa kilometa za mraba 66,000. Sri Lanka ina Pato la Taifa la Dola za Marekani bilioni 60 mwaka 2011, Tanzania Pato lake la Taifa ni dola za Marekani bilioni 24. Sri Lanka ina jumla ya watu milioni 20, Tanzania ina jumla ya watu milioni 45, Mkoa wa Lindi una jumla ya watu 750,000 hivi. Sri Lanka na Tanzania zote zina bajeti ya dola za Marekani bilioni tisa hivi. Uchumi wa Sri Lanka unategemea sana zao la chai na utalii kwa fedha za kigeni. Mkoa wa Lindi una eneo kubwa zaidi la Kilimo kuliko Sri Lanka nzima hasa ukizingatia katika hekta milioni 5.2 zinazofaa kwa kilimo ni hekta 500,000 tu ndio zinalimwa. Zao la korosho laweza kuwa chai ya Lindi. Kilometa za mraba 18,000 za Mkoa wa Lindi ni Selous Game Reserve, Kilwa ni kivutio kikubwa cha utalii wa kila namna na Mkoa wa Lindi una fukwe ambazo hazijawahi kuguswa tangu dunia iundwe na Mola.
Sri Lanka hawana gesi asilia. Lindi na hasa Wilaya ya Kilwa ndio mzalishaji mkubwa wa gesi asilia hapa nchini. Pia sehemu kubwa ya gesi iliyogunduliwa hapa nchini ipo katika Mkoa wa Lindi ingawa wengi wetu hudhani kwamba ipo Mkoa wa Mtwara. Lakini Lindi na Mtwara sawa tu. Mtwara ina kilometa za mraba 16,000 (chini ya eneo la Lindi lililopo Selous). Tufanye Lindi na Mtwara kwa pamoja ndiyo Sri Lanka ya Tanzania. Tunaweza kujenga uchumi wa dola za Marekani bilioni 60 kwa Lindi na Mtwara? Tunaweza kufanya mikoa hii iwe na kiwango cha umasikini chini ya asilimia tatu ya wananchi wake? Tunaweza kuingiza watalii 800,000 kwa mwaka kwa mikoa hii tu? Tunaweza kuuza nje korosho yenye thamani ya dola za Marekani angalau milioni 600? Tunaweza kutumia sehemu ya mapato yatokanayo na gesi asili kujenga miundombinu ya barabara, umeme, reli na maji kwenye wilaya zote za hii Sri Lanka yetu? Tunaweza kuwekeza kwenye elimu kuhakikisha kila mtoto anapata elimu bora? Tunaweza kuhakikisha kuwa asilimia 97 ya wakazi hii Sri Lanka yetu wanapata huduma za afya?
Majibu ya maswali yote haya ni NDIO. Utashi. Utayari. Uthubutu. Hebu tuthubutu kuiweka Sri Lanka Tanzania. Lindi na Mtwara ni zaidi ya Sri Lanka. Nikipata fursa ya kuandika tena nitaandika kuhusu uwekezaji kwenye elimu nchini Sri Lanka na kwamba haki ya kupata elimu mpaka Chuo Kikuu ni haki ya kikatiba yenye kuweza kudaiwa mahakamani.
Mwandishi wa makala haya Kabwe Zitto ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA na Naibu Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni.

No comments:

Post a Comment